Raila Odinga Uso kwa Uso na Uhuru Kenyatta

Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa Upinzani Raila Odinga wamekutana kwa mara ya kwanza tangu kufutiliwa mbali kwa matokeo ya uchaguzi wa urais wa Agosti 8 na mahakama ya juu.

Wawili hao pamoja na viongozi wengine ,wengi kutoka chama tawala cha Jubilee wamehudhuria mazishi ya aliyekuwa Meya wa Nairobi Samuel Mbugua , babake aliyekuwa mwakilishi wa wanawake katika kaunti ya Nairobi Rachel Shebesh katika shamba lake huko Kiambu.

Rais Kenyatta na Raila Odinga wamekuwa na misimamo mikali kuhusu marudio ya uchaguzi mkuu huku kiongozi wa Nasa akisisitiza kwamba mahitaji yake ni lazima yaafikiwe kabla ya uchaguzi mwengine kufanyika.

Miongoni mwa viongozi waliokuwepo ni gavana wa Kiambu Ferdinand Waititu na Seneta wa Nairobi Johnson Sakaja .

Hatua ya Odinga kuhudhuria mazishi hayo inaonyesha urafiki mkubwa ambao amekuwa nao na familia ya Mbugua.

Bwana Mbugua aliwahi kufanya kazi naye katika chama cha ODM.

Wakati huohuo ODM ilimteuwa bi Rachel Shebesh kuwa mbunge wake mwaka 2007 na 2012 kabla ya kujiunga na chama cha rais Kenyatta cha TNA 2012.

story@moodyhamza