Zlatan Ibrahimovic na Paul Pogba wataorodheshwa katika kikosi cha Manchester United

Zlatan Ibrahimovic na Paul Pogba wataorodheshwa katika kikosi cha Manchester United katika mechi ya Jumamosi ya ligi ya Uingereza dhidi ya Newcastle katika uwanja wa Old Trafford.

Mshambuliaji Ibrahimovic , 36, bado hajashirikishwa katika mechi yoyote msimu huu baada ya kupata jeraha la goti mnamo mwezi Aprili.

Kiungo wa kati Paul Pogba , 24, hajaichezea timu yake tangu alipopata jeraha la nyuma ya goti dhidi ya klabu ya Basel mnamo mwezi Septemba.

Beki Marcos Rojo pia anapatikana na mkufunzi Jose Mourinho alisema kuwa wote wataorodheshwa.

”Paul unaweza kuona. Unaweza kugundua kwamba kulikuwa na Manchester United msimu huu kabla na hata baada ya jeraha lake”, aliongezea Mourinho.

”Ana uwezo ambao hubadilisha vile tutakavyocheza mechi zetu”.

Mshambuliaji wa zamani wa Sweden Ibrahimovic ameichezea klabu hiyo mechi 46 na kufunga magoli 28 msimu uliopita.

Aliachiliwa na klabu hiyo mnamo mwezi Juni baada ya msimu wake kumalizwa na jereha la nyuma ya goti lakini akapewa mkataba mwengine mpya wa mwaka mmoja mnamo mwezi Agosti.

”Msimu uliopita tulimchezesha Zlatan kila dakika”, aliongezea Mourinho.

”Tulijifunza kucheza bila yeye.Lakini tunamkaribisha ni mchezaji mzuri sana”.

@moodyhamza