Wafanyabiashara wa madini wamwagiwa tindikali Arusha.

Moja ya taarifa niliyoipokea kutoka Arusha ni kuhusu Wafanyabiashara wadogo wadogo wanne wa Madini akiwemo Makamu Mwenyekiti wa wafanyabiashara hao, Ngalae Mapera kudaiwa kumwagiwa tindikali usoni na watu wasiofahamika.

Tukio hilo limetokea katika eneo la St Thomas, Arusha ambako watu wasiofahamika walifika katika eneo hilo wakiwa kwenye gari aina ya Rav 4 ya rangi ya Blue na waliposhuka waliwamwagia maji yanayosadikiwa kuwa na kemikali

Mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo Ole Laiser alisema baada ya gari kusimama walishuka wanawake wanne ambao hawakujulikana na kuwafuata wafanyabiashara hao kisha kuanza kubishana kuhusiana na masuala ya fedha.

>>>”Sisi tuliona baada ya wao kufika hapa waliegesha gari lao na kuwafuata wenzetu ambapo walikuwa wakibishana sana. Baada ya muda tulimuona mmoja wa wanawake akirudi kwenye gari tukajua ameenda kufuata bastola na baada ya muda alikuja ameshika chupa na kuwamwagia wenzetu.” – Ole Laiser.

Wafanyabiashara waliofikwa na tukio hilo ni Lucas Kiruswa, Sebastian Laiser, Moringe Issa pamoja na Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wadogo wa Madini Ngalae Mapera.

Kamanda wa Polisi Arusha, Charles Mkumbo amethibitisha kutokea tukio hilo na kusema Polisi wangali wanachunguza undani wa tukio hilo na watatoa taarifa kamili baada ya uchunguzi kukamilika.

Source: Teamtz