Hatimaye Acacia Gold Mine Yalipa Ushuru.

Mgodi wa dhahabu wa Acacia Bulyanhulu (BGML) uliopo katika Halmashauri ya Msalala, mkoa wa Shinyanga jana Jumatano Julai 26,2017 umekabidhi hundi yenye thamani ya Shilingi 460,732,841.08/= kwa ajili ya ushuru wa Huduma kwa halmashauri ya Msalala.

Akizungumza wakati wa kukabidhi hundi hiyo,Meneja Mkuu wa Mgodi wa Bulyanhulu Graham Crew alisema kiasi hicho ni asilimia 67 ya malipo ya ushuru wa huduma kwa ajili ya kipindi cha miezi sita kuanzia Januari hadi mwezi Juni mwaka huu ambacho ni asilimia 0.3 ya ukokotoaji wa ushuru wa huduma wa mgodi huo katika kipindi hicho.

“Jumla ya malipo ya ushuru wa huduma kwa kipindi cha miezi sita iliyopita ni shilingi za Kitanzania 687,660,956.84/=,ambapo malipo hayo yamegawanywa katika halmashauri mbili ambazo ni Msalala inayopata asilimia 67 na Nyang’wale iliyopo mkoani Geita inapata asilimia 33”,alifafanua Crew.

Alisema kutokana na mgawanyo huo,halmashauri ya Msalala imelipwa shilingi milioni 460 (460,732,841.08/= ) na Nyang’wale shilingi Milioni 226 (226,928,115.76/=.

“Ushuru umepungua kwa kuwa mgodi haujafanya mauzo ya makinikia ambayo yamezuiwa tangu mwanzoni mwa mwezi machi mwaka huu, hivyo tunafahamu kuwa tutalipa zaidi tutakapouza makinikia ambayo yapo yanaendelea kukusanywa mgodini”,aliongeza Crew.

Katika hatua nyingine Crew alisema tangu mwaka 2000 mpaka sasa mgodi huo umelipa zaidi ya shilingi 10,247,742,957/= za kodi ya ushuru wa huduma na kampuni ya Acacia ilianza kutoa malipo ya ushuru wa huduma wa asilimia 0.3 ya mapato ghafi kwa halmashauri husika mwaka 2014.

“Mgodi wetu unaendelea kuwa na matarajio ya kuchangia kuimarisha sekta ya viwanda kwenye uchimbaji madini katika halmashauri ya Msalala huku tukiendelea kutekeleza mkakati wa Jamii Endelevu wa Acacia ulioanzishwa mwaka 2016 kwa kushauriana na wadau lengo likiwa ni kuchangia maendeleo ya Jamii Endelevu inayonufaika na kukua kwa uchumi ndani ya jamii ili kujenga mahusiano ya kuaminika”,alisema Crew.

Akipokea hundi hiyo kisha kuikabidhi kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Msalala, Mkuu wa wilaya ya Kahama Fadhili Nkurlu aliushukuru mgodi wa Acacia Bulyanhulu kwa kuendelea kuunga mkono jitihada za serikali katika kutoa huduma kwa jami.

“Hiki kiwango cha shilingi milioni 460 tulichopokea ni kiwango kizuri ingawa kimepungua ulikinganisha na kipindi cha miezi sita cha Mwezi Juni hadi Desemba 2016,furaha inatujaza kwamba ile shilingi milioni 300 na zaidi ipo ndani ya Makinikia, yatakapouzwa tutaipata na tutaendelea kuboresha huduma za kijamii”,alieleza Nkurlu.

Nkurulu alimuomba mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala kuhakikisha fedha zilizotolewa na mgodi huo zitumike kwa huduma za kijamii kama zilivyokusudiwa ikiwemo kuboresha huduma za afya na miundombinu.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Msalala Simon Berege alisema mapato waliyopokea kutoka mgodi huo yako chini kwa shilingi milioni 300 ukilinganisha na kipindi kilichopita cha kuanzia Mwezi Julai hadi Desemba 2016 ambapo mgodi huo ulipokea shilingi milioni 760.

“Sisi tumepokea mapato haya kama tunavyopkea mapato mengine tunayopata katika halmashauri zetu,mapato haya ni yako chini ukilinganisha na kipindi kilichopita,tunaambiwa mapato yamepungua kutokana na Makinikia ambapo sasa yamesimama,hii inaleta changamoto katika ukusanyaji wa mapato katika halmashauri yetu, tunaamini mazungumzo baina Acacia na serikali yakiisha halmashauri yetu itapata mapato mengi Zaidi,” aliongeza Berege

Source:Udaku